Thursday, May 08, 2014
0
Mashirika ya kutoa misaada yameonya kuwa zaidi ya watoto 50,000 wa Somalia wenye matatizo ya utapia mlo wamo katika hatari ya kufa, miaka mitatu tu baada ya kipindi kibaya cha ukame kukumba taifa hilo.
Katika Ripoti inayoitwa ‘Risk of Relapse’ yani tisho la kurejea tena kwa njaa, mashirika hayo 22 yamesema kuwa hatua ya dharura inafaa kuchukuliwa ili kukabiliana na hali ilivyo na kuzuia uwezekano wa taifa hilo kurejea katika hali ya njaa.
Inasemekana kuwa karibu thuluthi moja ya Raia wa Somalia wanahitaji msaada.
Ingawa takwimu hizi zinaonyesha hali bora zaidi ikilinganishwa na miaka ya hapo nyuma ripoti hii inaonya kuwa hili halifai kuchukuliwa kuwa mafanikio.
Ed Pomfret, kutoka Shirika la kijamii la Oxfam amesema kuwa takwimu zilizo katika ripoti hiyo zinaweza kuwa za kutisha katika sehemu yeyote duniani.

Maafa

Zaidi ya watu 250,000 walifariki kufuatia njaa iliyosababishwa na ukame mwaka wa 2011.
Janga hilo liliathiri zaidi ya watu millioni kumi na tatu katika eneo la upembe mwa Afrika na kusababisha idadi kubwa ya wakimbizi , huku mamia ya maelfu ya wasomali wakitoroka maeneo yaliyo kuwa yanadhibitiwa na Al-shabaab.
Wanamgambo hao wa Alshabaab walikuwa wamepiga marufuku kusambazwa kwa chakula na mashirika kadhaa ya kijamii katika maeneo ambayo walikuwa wanadhibiti.
Imesema kuwa dola millioni 822 zaidi zinahitajika ili kugharamia mahitaji ya mwaka huu.
Pomfret ananukuliwa na shirika la habari la AFP akisema ‘Tatizo la Somali ni kuwa imekuwa na mgogoro kwa zaidi ya miaka 20, na hivyo watu wengi wanaipuuz kwa kudhani kuwa kule ni kwa magaidi, maharamia, njaa na kifo na hawawezi wakafanya lolote kuhusu hilo. Tusipochukua hatua sasa, kuna hatari kuwa hali ile inaweza kuzorota zaidi na kuwa janga.’
Tangu mwaka wa 1991 Somalia imeshuhudia vita vya kiukoo, wanasiasa na wapiganaji wa Kiislamu waking’ng’ania kudhibiti taifa hilo, hali ambayo imesababisha uasi na uharamia kustawi.
Hali ya utulivu imerejea kidogo katika baadfhi ya maeneo ya nchi hiyo kutoka mwaka wa 2012 ambapo serikali iliyoungwa mkono na umoja wa kimataifa iliwekwa.
Hata hivyo Alshabaab bado wanadhibiti miji mingi na maeneo ya kusini mwa Somalia.

0 comments:

Post a Comment

MAONI YAKO HAPA

Name

Email *

Message *

MARAFIKI

WANAO NITEMBELEA